Latest News

SAUT yakanusha vyuo vyake kuzuiwa kudahili


CHUO Kikuu cha Mtakatifu Agustino (SAUT), kimetoa ufafanuzi wa taarifa zinazosambazwa kwenye mitandao ya kijamii kuwa vyuo vyake vishiriki vimezuiwa na Tume ya Vyuo Vikuu nchini (TCU) kufanya udahili wa wanafunzi.
Taarifa hizo zinazosambazwa kwenye mitandao ya kijamii zimedai kuwa vyuo vishiriki vya SAUT ambavyo ni Stella Maris Mtwara University College (STEMMUCO) na Archbishop James University College (AJUCO) vimefungiwa na TCU kufanya udahili wa wanafunzi kwa mwaka wa masomo 2016/2017.
Kwa mujibu wa taarifa kwa vyombo vya habari iliyotolewa na Makamu Mkuu wa Chuo cha SAUT, Dk Thadeus Mkamwa, taarifa hizo ni za upotoshaji na kuwa hawajapokea taarifa kutoka TCU ikivizuia vyuo hivyo viwili kufanya udahili.
Aidha, Dk Mkamwa aliiomba jamii na wadau wa elimu kwa ujumla kupuuzia taarifa hizo kwa kuwa zina uwezekano wa kuwa ni mbinu chafu zinazofanywa na baadhi ya watu kuuhadaa umma hasa katika kipindi hiki ambacho ni muafaka kwa waombaji kufanya maombi katika vyuo vikuu.
Alisema SAUT ni Chuo Kikuu kinachomilikiwa na Kanisa Katoliki Tanzania, na kwamba kimepiga hatua kubwa katika kujiendeleza na kufanikiwa kuanzishwa kwa vyuo vingine vikuu vishiriki vya SAUT ambavyo ni STEMMUCO kilichopo Mtwara, AJUCO kilichopo Songea na Jordan University College (JUCO) kilichopo Morogoro.
Vyuo vingine ni St. Francis University College of Health and Allied Sciences (SFUCHAS)- Morogoro, Archbishop Mihayo University College (AMUCTA)- Tabora, na Cardinal Rugambwa Memorial University College (CARUMUCO) kilichopo Bukoba, Marian University College (MARUCO) kilichopo Bagamoyo. Dk Mkamwa aliongeza kuwa, chuo kimeweza kuanzisha vituo vingine vitatu vya SAUT vilivyoko Mbeya, Arusha na Dar es Salaam.

No comments:

Post a Comment

PERUZI24HOURS Designed by Templateism.com Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.